MZEE SUMAYE: RAIS SAMIA AMEFUNGUA MILANGO YA KIDIPLOMASIA
BABATI: Waziri Mkuu Mstaafu, Mzee Fredrick Sumaye amesema Rais Samia Suluhu Hassan amefungua milango ya kidiplomasia ambayo imechangia ushirikiano mzuri na mataifa mengine na kuchangia ongezeko la wawekezaji kutoka nje ambao wamewekeza katika sekta mbalimbali.
Sumaye ameeleza hayo leo Juni 4,alipopata nafasi ya kusalimia wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye viwanja vya Mollel Papaa Wilaya ya Babati mkoani Manyara katika ziara ya Katibu wa NEC itikadi Uenezi na Mafunzo wa CCM, Amos Makalla katika mikoa ya kaskazini.
Pia amesema Rais Samia amedumisha utulivu na amani katika nchi kwa kurudisha amani kwa wafanyabiashara wa ndani ambayo imekuwa ni moja ya kivutio kwa wawekezaji wengine kutoka nje.
Aidha, alisema hapo awali wafanyabiashara walifunga biashara zao na kupoteza matumaini lakini Rais Samia alirudisha utulivu amani na matumaini kwa watanzania na pia watanzania walikuwa wamefungiwa milango katika nchi za nje lakini Rais Samia alifungua milango ga kidiplomasia.
“Rais Samia alifungua milango ga kidiplomasia ya nje leo wageni wamejaa, watalii na wawekezaji wanaimani na Tanzania na wanakuja kwa wingi kuwekeza katika nchi yetu na watanzania tunaombwa tushirikiane nao kama ikiwezekana, mama Samia amefanya kazi kubwa sana kurudisha ushirikiano wa kimataifa,” amesema Sumaye.