UCHAGUZI MKUU SIO AJALI-WASIRA
*Asema waliokuwa wanafunga vioo vya magari wajue sasa wanarudi kwa wapigakura
*Ashauri wanaotaka kugombea ubunge
wapime kina cha maji kabla kuingia
Na Mwandishi Wetu, Mwanza
MAKAMU Mwwnyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Bara, Stephen Wasira amewaeleza wabunge na madiwani hususan waliokuwa wanajifungia vioo kwenye magari wajue wakati umefika.
Amesema uchaguzi mkuu sio ajali na kwamba wabunge na madiwani wanajua kila baada ya miaka mitano hufanyika uchaguzi mkuu.
Aidha, amewaeleza wana CCM wanaotaka kugombea ubunge na udiwani ni vema wakapima uwezo wao kama ambavyo unapaswa kupima kina cha maji kwa fimbo kabla ya kuvuka mto kusombwa na maji.
Akizungumza na viongozi na wanachama wa CCM katika Wilaya ya Magu mkoani Mwanza, leo Juni 23, 2025, Wasira ametumia nafasi hiyo kuwataka wana CCM kujiandaa kwenda kutiki ifikapo Oktoba na kwa nafasi ya urais tayari Chama kimepitisha jina la Dk. Samia Suluhu Hassan na mgombea mwenza ni Dk. Emanuel Nchimbi.
“Kwa upande wa urais tumemaliza tumeshaweka mgombea wetu Dk.Samia Suluhu Hassan na kazi yetu ni kumuuza kwa wananchama na wananchi .Kwa wabunge kama ubunge unaisha Juni 27 ndio maana hauwapi presha maana tangu walipoingia walijua ikifika miaka mitano uchaguzi unafanyika.
“Kwa hiyo uchaguzi sio ajali... kama wewe unauogopa labda hukufanya maandalizi maana wako watu katika jamii hata wale waliowachagua hawawajui wale ndio wenye kupata presha... sasa kama unafunga vioo unawapita watu usilaumu watu,” amesema Wasira.
Ameeleza zaidi kuwa, amekuwa mbunge kwa miaka 30, hivyo analijua bunge vizuri na kueleza kwamba unapatikana kwa kujenga uhusiano na watu, "ukijenga uhusiano na watu mambo yako yanakuwa rahisi."
Akizungumza zaidi Pia Wasira alisema uchaguzi umefika na wanachama wana haki ya kuchukua fomu ila alishauri kwa wale wanachama wapya wanaotaka ubunge wakapima nguvu ya waliopo au waliomaliza muda wao.
“Wakati sisi zamani tukiwa watoto ukitaka kuvuka mto maana madaraja hayakuwepo na mito kama inatiririka hivi unaenda na fimbo, unatanguliza fimbo uone kama fimbo itatikiswa na maji, ikitikiswa na maji mpaka take kwenda huingii pale maana utaenda wewe,
“Nataka wenzangu niwaambie wanaotaka ubunge hakuna mtu anawazuia hata kidogo, ushauri wangu watembee na fimbo kwanza wapime kina cha maji wakiona kina ni kigumu wasubiri hadi mto upungue sasa sijui kama utapungua kabla uchaguzi, huo ni ushauri,”alisema Wasira.